NISITIRI: Nina Vipande vya Maisha Vilivyopotea

Wanayopitia Mabinti katika Ubinti wao!

Maisha yangu yamejaa uchungu na aibu” ….. Batuli Mwinyiheri

“Ninatamani kuendelea na masomo lakini nashindwa kutokana na hali halisi ya maisha yangu na wazazi wangu.

Nina umri wa miaka 14, baba yangu mzazi alishafariki na mama yangu aliolewa na mwanaume mwingine. Mume wa mama yangu, yaani baba yangu anayenilea sasa amekuwa akinitesa japo kama hupitii ninachopitia huwezi kuamini kama ananitesa. Mbele za watu anaonekana kutujali mimi na mama lakini sivyo ilivyo katika maisha halisi tunayoishi nyumbani kama familia.

Mama yangu amekuwa dhaifu kiafya kwa muda wa miaka miwili sasa. Anasumbuliwa na mgongo kutokana na kupigwa na baba. Mimi ndiye nimekuwa nikimtunza mama hasa nyakati za mchana ambapo baba anakuwa amekwenda shambani.

Nimeshavunja ungo. Nikiwa katika siku zangu huwa ninapata maumivu makali sana ya tumbo, mgongo, kiuno na kichwa. Katika kipindi kama hiki, siwezi kuvuka kizingiti cha mlango kwa sababu damu inachuruzika sana na sina kitu cha kuweka ili isipitilize.

Nguo zangu zimechakaa zote hadi sasa navaa nguo za shule hata ninapokuwa nyumbani nikimuuguza mama.

Mimi ndiye nafanya kila kazi nyumbani. Naamka saa kumi na moja asubuhi ili nikateke maji, nirudi nichanje kuni, nisafishe uwanda wa nyumba, niandae kifungua kinywa. Nimuogeshe na kuhakikisha amekula vizuri.

Nikitaka chochote kutoka kwa baba hata kama ni kwa ajili ya chakula anasema ni lazima nilipie. Nikimwambia sina hela anafanya tendo la ndoa na mimi kwanza ndipo anipe ninachohitaji. Wakati mwingine ananifanyia hivyo na asinipe ninachohitaji. Mara nyingi ananiambia inabidi nimsaidie mama yangu kwani alimuoa kwa ajili hiyo. Sijawahi kumwambia mama kwani najua ataumia sana. Naona kabisa maisha yangu yanavyopotea.

Nakushukuru sana nimeongea na wewe. Naomba unisaidie mama yangu apone. Akipona nitafurahi sana. Mama akipona najua nitarudi shule. Lakini pia naomba unisaidie nipate vitambaa vya kuweka nikiwa kwenye siku zangu.”

Nisitiri – DhaminiHedhi Kampeni

Nisitiri – Dhamini Hedhi ni kampeni yenye lengo la kuwafikia mabinti elfu moja kutoka kwenye familia zenye changamoto ya kiuchmi kiasi cha kushindwa kutimiza hitaji la kununuliwa taulo za kike.

Lengo la kampeni hii ni kuwasitiri mabinti hawa wanapokuwa katika hedhi ya mwezi kwa kuwasaidia kupata taulo za kike.  Kama tunavyojua, mwanamke anapokuwa katika hedhi kuna damu inayokuwa inatoka kwenye mwili wake kupitia viungo vyake  za uzazi.  Katika kipindi hiki mwanamke anahitaji kuwa amesitirika ili kwamba ile damu inayotoka kipindi hicho isipitilize na kuonekana kwa nje na mtu mwingine.  Hedhi ni jambo la staha, damu inayotoka inapaswa kuonwa na anayetokwa damu tu na si vinginevyo.  Mwanamke au binti anahitaji taulo za kike kwa ajili ya kujisitiri katika kipindi hiki.

Hedhi ni jambo la asili.  Hedhi ni jambo la uumbaji lililofanywa na MUNGU mwenyewe.  Kila mwanamke aliye kamili huwa na vipindi vya hedhi baada tu ya kuvunja ungo. Hedhi sio jambo ambalo mtu anaweza kuchagua kuwa nayo au kutokuwa nayo.

Inapotokea kwamba, mwanamke au binti yeyote anashindwa kujisitiri katika kipindi hiki cha hedhi, maisha yake hujaa simanzi na unyonge; ujasiri wote humuishia kwani anakuwa katika hali ya mashaka kwamba huenda akachafuka muda wowote kwa damu inayokuwa ikimtoka mwilini mwake kupitia viungo vyake vya uzazi.  Hii damu inapotoka haitoi ishara ya namna yoyote kama vile unapokuwa unasikia haja ndogo au haja kubwa, hii hutoka tu.

Katika mazingira kama haya, binti anapokosa taulo za kike kwa ajili ya kujisitiri kwenye kipindi hiki cha hedhi inamwia vigumu sana kufanya jambo lolote ikiwemo kuhudhuria masomo.

  • Ili mwanafunzi ahudhurie ipasavyo masomo yake anatakiwa ahudhurie siku 194 na vipindi 1740 katika mwaka mmoja wa masomo.
  • Lakini kwa mtoto wa kike hasa wa kijijini amekuwa akikosa masomo kwa wastani wa siku 84 kwa mwaka kutokana na suala la hedhi ambalo ni suala la kimaumbile.
  • Jambo hilo humfanya msichana kukosa kuhudhuria vipindi 756 vyenye Dakika 40 kila kimoja.
  • Hii ni kutokana na changamoto ya kipato cha wazazi wao na pia shule nyingi nchini hasa za vijijini kutokuwa na mazingira rafiki ya usafi kwa wanafunzi wa kike.

Kupitia NISITIRI – Dhamini Hedhi kampeni tunaungana pamoja na serikali, mashirika mbalimbali na jamii kwa ujumla kuhakikisha mtoto wa kike anapata vihifadhi hedhi, yaani taulo za kike, kwa ajili ya kujisitiri katika mzunguko wake wa mwezi lakini pia anapata elimu na uelewa zaidi kuhusu Hedhi salama.

Lengo la kampeni hii ni kuwafikia mabinti elfu moja wanaokaa vijijini. Ni kampeni ya miezi mitano kuanzia 01.02.2020 hadi 30.06.2020. Paketi moja ya taulo za kike itamwezesha binti mmoja kuwa na uhakika wa kuishi bila hofu ya kutokusitirika wakati wa hedhi yake ya mwezi kwa muda wa miaka miwili. Paketi moja inapatikana kwa gharama ya TZS. 10,000/- . Aina ya taulo za kike tunazotegemea kuwapatia ni zile ambazo anaweza kuzifua baada ya kuzitumia. Unaweza kuchangia kupitia https://www.wezeshasasa.com/nisitiri-dhamini-hedhi

Kiwango chochote kuanzia shilingi 1,000/- za Kitanzania.

Asante sana. Karibu ushiriki kwenye kampeni hii yenye mashiko kwa maisha ya binti.