MAFANIKIO YENYE USHAWISHI – II

ASILI YA MAFANIKIO

Katika mafanikio kuna vitu viwili ambavyo usipovielewa vinafanyaje kazi katika kuchangia wewe kupata mafanikio yako, utachanganyikiwa.  Vitu hivyo ni Sheria na Kanuni.

Fahamu:  Kuna sehemu ya Kanuni katika mafanikio au kutokufaniniwa kwa mtu binafsi na kuna sehemu ya sheria katika mafanikio au kutokufaniniwa kwa mtu binafsi.

Tofauti ya Sheria na Kanuni

Sheria zinaweza kukuzuia kufikia mafanikio unayotaka kuyafikia.  Yeyote anayetaka kufanikiwa ni lazima avunje sheria za maisha.  Kushindwa kwako katika maisha kunasababishwa na kitendo chako cha kuamua kuwa unatii sheria za maisha.  Usichanganye Sheria na Kanuni.

Kanuni za maisha

Kanuni za maisha hazifanyi kazi kulingana na kile ulichowahi kupitia katika maisha yako au unachopitia sasa, hapana.  Zinafanya kazi wakati wote, haijalishi kama unajua uwepo wa hizo kanuni au hujui.

Mafanikio yanatabirika na kushindwa pia kunatabirika kwa sababu kila kitu katika maisha kiliumbwa kufanya kazi kwa kanuni.  Kanuni huyafanya maisha kutabirika.  Kila kitu kina kanuni inayoambatana nacho kwa sababu kila alichoumba MUNGU kinapaswa kufanikiwa. Kila kitu kinafanikiwa kwa kufuata kanuni.  Kila mtu anafanikiwa kwa kufuata kanuni. 

MUNGU alimuumba mwanadamu kwa ustadi wa kiwango cha hali ya juu sana.  MUNGU aliweka kanuni ambazo endapo mwanadamu atazifuata ni lazima atafanikiwa.  Chochote alichokiumba MUNGU ni lazima kifanikiwe.  Mafanikio ni jambo zuri mbele za MUNGU.

Mafanikio ni muhimu.  Ukitaka kufanikiwa katika maisha usijaribu kufanikiwa katika maisha.  Watu wengi wanashindwa kufanikiwa kwa sababu wanajaribu kufanikiwa.  Watu waliofanikiwa hawakujaribu kufaninikiwa, walitekeleza kwa vitendo kanuni za mafanikio na kanuni za maisha.  Kwa maneno mengine, mafanikio ni matokea ya kuwa mtiifu kwenye kanuni.

Mafanikio ni matunda ya shughuli unayojihusisha nayo yaliyotokana na wewe kufuata kanuni.

Unajuaje kama umefanikiwa?

Mafanikio hayapimwi kwa kulinganisha jambo ulilofanya wewe na alilofanya mtu mwingine kwani siku zote wapo watu uliowazidi na waliokuzidi pia.  Mafanikio yanapimwa kwa kulinganisha kati ya kile ulichofanya na kile unachopaswa kufanya.  Mafanikio yanapimwa kupitia nia ya msingi ya wewe kufanya hicho unachofanya.  Mafanikio yako hayapimwi kutokana na kile ulichofanya, hapana, mafanikio yako hupimwa kutokana na lile kusudi la MUNGU kukuumba.  Mafanikio ni utimilifu wa kusudi la MUNGU juu ya maisha yako.  Mafanikio katika maisha yako yanachochewa na kusudi la MUNGU juu ya maisha yako, yaani kile kitu ambacho MUNGU alikuumba uje kukitimiza hapa duniani.  Mafanikio ni kutimia kwa mpango wa MUNGU juu ya maisha yako. Kuna kusudi MUNGU ameweka ndani yako na kuna mahali MUNGU anataka ufike. Haijalishi ni watu wangapi watakusifia, watakushangilia na kukupongeza, kama hukufanya kile kitu ambacho MUNGU anataka ufanye na kama hukufika pale ambapo MUNGU anapotaka ufike, wewe hujafanikiwa. Mafanikio ya Kiungu yanapimwa kwa kufikia ile hatima ambayo MUNGU amekukusudia.  Maisha sio kwa habari ya kufanya kazi kwa bidii lakini kufanya kazi kwa werevu na uhodari kwa kutumia maarifa sahihi.  Utaweza kufanya kazi kwa werevu ukiwa na maarifa yaliyofichwa kwenye kanuni. Chochote unachoanza kufanya au unachoacha kufanya kinategemea zaidi na kanuni unazozifuata au kutozifuata. Kufanikiwa kwako au kushindwa kwako kunategemea na kanuni za maisha unazotii au kutokutii.   Mafanikio sio suala la MUNGU bali ni juu yako wewe mwenyewe.

Mafanikio ni mchakato.  Mafanikio yanavutiwa zaidi na wewe kuwa unaenenda katika mwelekeo sahihi kuliko wewe kufika pale unapokwenda.  Mafanikio ni ule mchakato unaoupitia kuelekea kule unakotakiwa kufika na sio kufika kule unapotakiwa kufika.  Yaani mafanikio yanapatikana hapa njiani kwenye safari ya kuelekea kule unakotaka kufika.  Ukifanikiwa kwa kupitia mchakato sahihi unakuwa umetimiza kusudi lako.

Kama huzijui kanuni za hicho kitu unachotaka kufanikiwa ni dhahiri kwamba hutaweza kuzitii hizo kanuni, Unaposhindwa kuzitii hizo kanuni huwezi kufaninikiwa.  Haijalishi utajibidisha kwa kiwango gani au utamwomba MUNGU kwa kiasi gani.  Mafanikio ni matokea ya kutii kanuni.

Mafanikio yenye ushawishi ni yale yanayofuata kanuni.

—– Tutaendelea wiki ijayo.